Saturday, 7 February 2015

KATIBA MPYA, KIGEZO CHA SHAHADA KWA MGOMBEA URAIS SASA KUTUPATIA RAIS BORA .




NA  BASHIR  YAKUB (MWANASHERIA  MWANDAMIZI)

Ni siku muhimu tena katika uchambuzi wa Ibara mbalimbali katika rasimu inayopendekezwa ili  ikipita iwe  katiba. Upo umuhimu mkubwa sana kwa Watanzania kujua kilichomo ndani ya  rasimu hii kwakuwa  leo hii inaitwa rasimu lakini kesho itaitwa sheria  na kila mtu anayejua kilichomo na asiyejua wote watalazimika kuwajibika kwake bila kukiuka .

Kwa msingi huu elimu na hamasa zaidi inahitajika ili kumfanya kila  mtu aone hili linamhusu kabla ya kuanza kulalamika kwa kuonewa itakapoanza kutekelezwa kwa lazima. Katika mwendelezo wa uchambuzi wa Ibara zilizomo katika rasimu  leo tujikite katika Sura ya  Nane Sehemu ya Kwanza ( b ) Ibara ya 85 ( 1 ) ( e )  ambayo inanukuliwa hivi

“Mtu atakuwa na sifa ya kuchaguliwa kushika  nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano ikiwa anayo shahada ya chuo cha elimu ya juu kinachotambuliwa kwa
mujibu wa sheria, au awe na ujuzi na uzoefu wa uongozi katika
ngazi ya taifa utakaomwezesha kumudu madaraka ya Rais”

Ibara ya namna hii  ni mara ya kwanza kabisa katika historia ya nchi yetu  kuingia katika katiba. Pamoja na mabadiliko mengi yaliyowahi kufanyika kwenye katiba kigezo hiki hakikuwahi kuingizwa.

Siwezi kusema  waliopendekeza  ibara hii kuwemo walilenga nini lakini  kwa akili ya kawaida  kabisa utaona kuwa wamezingatia zaidi mabadiliko makubwa ya kidunia. Hapo awali  sifa ya kuwa mgombea urais ilikuwa uwezo wa kujua na kusoma na kuandika. Aliyejua kusoma na kuandika  na sifa nyingine  ilimtosha kuizuru tume tayari kwa kuchukua fomu ya nafasi ya rais.

Leo rasimu ikipita  ina maana hata  mwenye stashahada(diploma) haruhusiwi kuusogolea urais.
Aidha ukiisoma vizuri ibara utaona kuwa hata stashahada ya juu ( Advanced diploma) ambayo  kwa mwenendo wetu wa elimu imekuwa ikichukuliwa kuwa na hadhi sawa  na shahada(degree) imekataliwa katika kuukwaa urais.

Kitu kingine ambacho kimejitokeza katika ibara hiyo ni  pale inapoainishwa sifa nyingine ambayo  ni ujuzi na uzoefu  wa uongozi katika ngazi ya taifa  utakaomwezesha kumudu madaraka ya rais.  Ibara imekaa hivi,  kwanza awe na shahada  ya kwanza  kutoka chuo kinachotambulika  au awe na uzoefu na ujuzi katika uongozi ngazi ya taifa wa kumwezesha kumudu madaraka ya rais.

Nimekariri hilo neno “au” hapo juu kwakuwa lina maana kubwa katika  ibara hii. Maana  ya neno au ni kuwa  anayeutaka urais awe na kimoja kati ya  elimu ya shahada au  uzoefu.  Hii maana yake ni kuwa inawezekana ukawa hata  na elimu ya darasa la saba  lakini ikiwa unao uzoefu  katika uongozi wa taifa basi umepata sifa kikatiba  ya kugombea.

 Ingekuwa  imesema awe na shahada  pamoja na uzoefu basi  ingekuwa maana yake vinatakiwa vyote viwili lakini kumbe  hata kimoja tu elimu au uzoefu  inakuwa tayari ni sifa  kwa mujibu wa ibara hii. Ufafanuzi wetu hapa huwa ni ufafanuzi wenye uwiano(balanced description). Huwa inaelezwa ibara  kama tulivyoona hapo juu halafu zinaelezwa faida zake na hasara zake ili iwe nafasi kwa msomaji mwenyewe kwa kutumia akili kuona lipi jema kwa mustakabali wa leo na kesho katika taifa na lipi si jema.Hivyo basi hapa chini zinaelezwa faida na hasara za Ibara hii.

FAIDA  AU  UZURI  WA IBARA  HII.

( a ) Kwanza kabisa kwa kuweka kigezo cha elimu  ya kiwango cha juu kama shahada  ibara hii  imezingatia sana hatua kubwa ambayo dunia imepiga. Ukweli ni kuwa uendeshaji wa nchi wa sasa  ni uendeshaji unaohitaji uelewa mkubwa unaotokana  pamoja na mambo mengine na kiwango kikubwa cha elimu  kama shahada.  

Yapo mambo makubwa ya  kitaalam yanahitaji ukokotozi na uelewa wa hali ya juu kwa mfano  mambo ya miamala ya kodi, sheria za kimataifa, mikataba mikubwa, upangaji wa sera  makini, uwezo wa kutafiti  na kuendana na mabadiliko makubwa ya kiteknolojia n.k.

Hayo yote yanahitaji shule kubwa   kwa hili wala tusiongee sana.  Ni kweli rais anakuwa na wasaidizi wake ambao kimsingi ndio wataalam haswa. Lakini hilo haliondoa ulazima wa yeye kutakiwa kujua mambo hayo pia. Hii ni kwakuwa pamoja na mambo kufanywa na wasaidizi mwisho wa siku lazima naye apitie na atoe ushauri, amri au maagizo kuhusiana nayo. Atawezaje kutoa maagizo kwenye mikataba mikubwa ya kiamataifa au jambo kubwa linalohusu sera  za nchi bila kuwa na elimu kubwa.

Atashauri nini kama hajui. Si atakuwa wa kudanganywa na watendaji na mwisho wa siku taifa linaangamia. Huo ni ukweli mtupu  na hakuna namna ya kuusema isipokuwa hivihivi ulivyosemwa.  Kwa ufupi twaweza kusema kuwa kwa ibara hii tutampata rais mweledi( professionalism)  na huu ndo utakuwa uzuri wa kwanza wa ibara hii.

( b )Faida au uzuri mwingine wa ibara hii ni kuwa  kwa kusema kuwa mtu awe na shahada  au ujuzi na uzoefu katika uongozi ibara imejitahidi kuwaingiza watu  wengine ambao hawatakuwa na shahada lakini wamekuwa katika uongozi kwa ngazi ya taifa kwa muda mrefu, wamekuwa waadilifu na wanao ujuzi wa kutosha  wa kuwawezesha kushika kiti cha rais.

Ni ukweli kuwa kuwa ndani ya serikali wamo watu wengi ambao hawana hizi shahada lakini wamekuwa katika uongozi wa taifa kwa muda mrefu  na wanao ujuzi wa kuongoza pengine kuliko hata hao wenye shahada zao. Tunao wanasiasa wengi wakongwe  ambao wengi wao kutokana na kusoma zamani au  vinginevyo  hawana  shahada lakini ni wazuri sana  katika uongozi. Wapo wengine waliwahi kuwa mawaziri huko nyuma, makatibu wakuu, wabunge na nyadhifa nyingine nyingi. Hawa nao wamepewa nafasi na ibara hii kwa sifa yao ya ujuzi na uzoefu.

0784482959
0714047241




Share this article :

0 comments:

Post a Comment