Saturday, 7 February 2015

WAKULIMA, WAFUGAJI,WAVUVI NI HAKI SASA KUISHITAKI SERIKALI WASIPOTENGEWA MAENEO MAALUM, KATIBA MPYA


NA  EMMANUEL  MARWA  ( WAKILI  MAHAKAMA  KUU).

Rasimu inayopendekezwa ili  iwe katiba inayo mambo mengi mapya.  Ni sahihi kusema mapya  kwakuwa  ni mambo ambayo hayapo katika  katiba yetu tuliyonayo  sasa. Moja ya mambo hayo  ni hili la kuingiza  au kuweka  haki za  wafugaji na wakulima, wachimbaji na wavuvi. Haya  ni  makundi muhimu sana katika jamii yetu  hasa kutokana  na ukweli  kuwa mpaka sasa  kundi  kama la wakulima  ndilo linaloonekana kubeba asilimia kubwa ya watu wote katika nchi hii.
Kwa ukweli kama huu kupata  katiba au  sheria ambamo  haki na  mustakabali wa watu kama  hawa unatajwa    si jambo la kubeza.  

( a ) MALALAMIKO   YA   MAKUNDI  YA  WAKULIMA, WAFUGAJI, WAVUVI,  WACHIMBA  MADINI.

Kwa  muda mrefu sasa  kumekuwepo  na malalamiko  kutoka kwa  makundi  hasa ya  wakulima  , wafugaji na wachimba  madini.  Malalamiko yao makubwa wamekuwa  wakiyaelekeza kwa serikali  na kubwa  zaidi wakiilalamikia  serikali kutokuwa na sera maalum ya kuwatengea  maeneo ya  kulima, malisho, kuvua  pamoja  na  maeneo  ya kuchimba madini.

Hali hii haikuwa imeishia katika malalamiko tu bali ilishapiga hatua  na  kuwa  mgogoro mkubwa  ambao sasa ulikuwa unaelekea kuwa janga la kitaifa. Na hali ilikuwa inakuwa mbaya  zaidi pale makundi haya yanapoanza  kugombea maeneo  kwa mfano  tumeshuhudia  mara kwa mara tena katika maeneo mbalimbali ya  nchi  kundi la wakulima  na kundi la wafugaji  wakigombea maeneo.

Hali ilikuwa tete  hasa pale ilipokuwa ikiripotiwa  vifo  na majeruhi kutokana  na magomvi  hayo. Tatizo kubwa ilikuwa ni kukosekana  kwa hiki ambacho  sasa kinaelezwa na rasimu hapa  chini.

( b ) WAKULIMA, WAFUGAJI, WAVUVI, WACHIMBA MADINI  KUTENGEWA MAENEO  YAO   RASMI.

Ibara  ya 46 ( 2 ) inasema kuwa  Mamlaka ya nchi itaweka utaratibu wa kisheria kwa madhumuni ya kubainisha na kutenga maeneo ya ardhi kwa ajili ya matumizi ya  kundi la  Wakulima, wafugaji, wavuvi na wachimbaji madini. Ibara  kama hii ni ibara  muhimu  kwa mustakabali wa  uchumi na amani ya  nchi yetu.Makundi ya jamii hizi  ni makundi  ambayo yamekuwa  yakiongezeka  kwa kasi ya ajabu.

Hatari kubwa ambayo imekuwa  ikitukabili kama taifa ni kuwa  wakati makundi ya wakulima, wafugaji na wavuvi yakiongezeka  kwa haraka mno  ardhi tuliyonayo imekuwa ikibaki ileile. Hii ni kusema kuwa mahitaji ya ardhi yanaongezeka wakati ardhi haiongezeki. Kwa usemi huu  kila mtu anaweza akapima hatari ambayo kama taifa tulikuwa tunaanza kukabiliana nayo.

Ni  bomu kubwa lililokuwa  likijitega taratibu. Kutokana na hali  kuwa  hivi  ilikuwa  basi  inahitajika sera madhubuti ya kudhibiti hali hii. Na sera  ya kudhibiti hali kama hii haikupaswa kuwa  sera ya kawaida.  Ilitakiwa  kuwa sera inayotokana  na sheria kuu kama katiba. Na  hiki  ndicho  kilichofanyika.Pamoja na hayo zipo haki nyingine za makundi haya kama  tutakavyoona hapa chini.

( c ) SASA  NI LAZIMA  WAKULIMA, WAFUGAJI  KUPEWA  TAARIFA  KUHUSU  SHUGHULI   ZAO.

Ibara hiyohiyo ya 46 (b) inazidi kusema kuwa wakulima.wafugaj,wavuvi na wachimba madini watakuwa na haki ya  kupata taarifa na maarifa kwa lengo la kuboresha kilimo, ufugaji, uvuvi na uchimbaji madini.Hapo juu  tumeona haki ya makundi haya kutengewa maeneo maalum. Hapa sasa tunaona haki yao  ya kupata taarifa  ikiwa ni pamoja na maarifa.

Taarifa maana yake  ni kuwa serikali sasa inalazimika kuweka mitandao  ya kuwapasha habari wakulima, wafugaji na wachimba madini kuhusu shughuli zao. Kwa hiyo kuwapasha habari  si hiyari tena isipokuwa lazima maana ni takwa la kikatiba.

Kwa upande wa maarifa  ni kama kuwaaandalia semina, majukwaa  ya mijadala ya kielimu,kuwaunganisha  na shule za kilimo,mifugo na uvuvi, vipeperushi na vijarida na kuwaandaa kwa kila kitu kuhusu elimu. Hili nalo si la hiyari tena kwakuwa litakuwa kikatiba.

( d ) WAKULIMA, WAFUGAJI,  WACHIMBA  MADINI  NA  HAKI   YA   KUMILIKI ARDHI.

Ibara hiyohiyo ya 46 ( a ) inawapa tena  wakulima, wafugaji,wavuvi, wachimba madini haki ya kumiliki ardhi kwa  kusema kuwa (a) wakulima, wafugaji,wavuvi, wachimba madini watakuwa na haki ya kumiliki, kutumia na kuendeleza ardhi kwa ajili ya shughuli zao;    
Kama Watanzania wengine  haki  ya kutumia  na kumiliki ardhi  walikuwa nayo hata kabla ya rasimu hii.
Lakini sasa kuiweka katika Katiba  na huku ikiwarejea wao peke yao  ni jambo la mafanikio  na  linaloonesha ni kwa namna  gani  ipo ari  ya kushughulikia matatizo yao.  Pia inaonesha ni kwa kiasi gani  makundi haya sasa yanatambulika rasmi  na haki zao zinatofautishwa  na haki za makundi mengine.

( e ) UMUHIMU  AU  FAIDA  KATIKA  IBARA  HIZI  JUU.

Kuna kitu kikubwa kimoja ambacho kinajitokeza  na kuwa kama faida kubwa ya ibara  nilizoeleza hapa juu. Kutokana na ibara kuwa katika mtindo huo tuliouona hapo juu  sasa ieleweke wazi kuwa  makundi  yote yaliyotajwa katika ibara  hizi  yamepata  ruhusa  ya  kuifungulia  mashtaka serikali  iwapo lolote katika  yaliyoorodheshwa kama haki  zao  hayakutekelezwa.

Hii ina maana  baada ya kupita kwa rasimu na  kuwa katiba wakulima, wavuvi, wachimba madini wasipotengewa maeneo maalum kwa ajili ya shughuli zao  basi  wanaweza kuishtaki serikali  kwa maombi maalum( petition)  na wakapata haki  hizo  ikiwemo fidia.  Kwa hiyo sasa ni kusema kwamba suala la serikali kutenga maeneo maalum kwa ajili  ya  makundi  haya  sasa ni la  lazima.
 0784482959, 0714047241



Share this article :

0 comments:

Post a Comment