Friday, 6 February 2015

URAIA WA NCHI MOJA :KUPUNGUZA UHALIFU NCHINI, KATIBA MPYA




NA  MAWAKILI  WETU-

Tunapita katika kipindi ambacho kama umakini, ukweli  na weledi utazingatiwa  taifa laweza kuwa kati ya mataifa tulivu yaliyostaarabika  katika nyanja za siasa, uchumi na jamii. Kinyume chake  ni taifa la visasi,mivutano, lisilojali utu haki za msingi na linaloendeshwa  kinyume na ustaarab wa dunia. Kulifikia hili umakini unatakiwa kutoka  kila upande, upande wa watawala na watawaliwa pia. Lakini kwa upande wa watawaliwa unahitajika umakini wa zaidi na wa ziada   kwasababu upande wao ni wa kupoteza, ni upande mbaya , upande dhaifu. Ubaya wa upande huu unatokana na sababu za kusababishiwa na za kusababisha.Nazumgumzia za kusababisha. Watawaliwa wananchi wana utamaduni wa miaka mingi wa kutopenda kufuatilia mambo yao wenyewe mpaka mambo hayo yawe ajenda za wanasiasa. Leo tuna habari ya rasimu ya katiba, haishangazi kukuta kati ya ibara 189 zilizo kwenye rasimu mtu hajawahi kuona hata ibara moja iwe kwenye gazeti au pengine popote. Anasubiri kulalamika atakapokuwa anapata huduma mbovu zinazotokana na kupitishwa kwa Ibara hizo.Ni rahisi na kawaida kwa baadhi ya watu kuhisi hawahusiki, na  hili likijitokeza tena katika mchakato huu basi itakuwa hatari na msiba. Hayumkini haitapita mda mrefu  walewale walioona jambo hili haliwahusu watakuwa wa kwanza kabla ya mwingine yeyote kugundua kuwa walikosea sana  na kuwa jambo hili lilikuwa linawahusu tena pengine sana kuliko  wale waliofikiliwa  kuwa ndio wahusika. Hata hivyo itakuwa haina maana  kwakuwa  watakuwa nje ya mda( time bared) na hakutakuwa na uwezo wa kufanya lolote isipokuwa kusikilizia maumivu tu.                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                              
                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                             
Nimewahi kujiuliza unaweza kutumia njia gani ili kuvuta umakini wa watu. Nilipata majibu lakini sikurudhika nayo. Sikuridhika nayo kwa kuwa  majibu  niliyopata  yalishafanyiwa kazi  sana lakini hakukuwa na mwitikio chanya. Ni hatari.
Mchakato wa katiba ni maarufu sana lakini amini usiamini unahusisha watu wachache sana.Tuko milioni 45 isikushangaze kukuta wanaofuatilia na kushiriki hawafiki hata milioni moja. Hii ni kuanzia utoaji wa maoni , ufuatiliaji wa lililokuwa bunge la katiba na ufuatiliaji wa jumla wa mchakato huu. Walio wengi hupenda kuhadithiwa, au kusikiliza  wadau wao katika siasa na hufanya  mawazo ya wadau wao kuwa yao. Hupenda wanasiasa watafakari kwa niaba yao. Watu huuza tafakari zao kwa wanasiasa, ni hatari.
Anayetaka kubadilika anaweza kuanza sasa kwa kufuatilia safu hii ambayo itakuwa ikileta maelezo na uchambuzi wa ibara mbalimbali muhimu katika rasimu ya katiba inayopendekezwa mpaka mchakato utakapokwisha. Mazingatio ni kuwa uchamnbuzi huu  hautakuwa wa upande wa ndio au hapana , Ukawa au CCM  isipokuwa utajikita katika hali halisi  ili itoshe  na iwe fursa ya mtu kufikiria mwenyewe. Uchambuzi utakuwa katika maelezo mepesi yenye kueleweka  hasa yakilenga watu wa kada ya kati na chini  ambao haswa ndio  husaidiwa na wanasiasa kufikiri. Nitakuwa nikieleza ibara  zenye maudhui yanayofanana  kwa wakati mmoja na hiyo ni kusema kuwa leo  tunaanza na Sura ya sita Ibara za  65,66,67,68 na 69.Ibara hizi kwa pamoja zinazungumzia Uraia  wa Jamhuri ya Muungano.


URAIA  NININI.
Uraia ni utambulisho. Wakati mwingine uraia huenda na nasaba lakini si lazima. Uraia zaidi ni utambulisho tu, ni kuwa fulani ni wa sehemu fulani basi.Si lazima uwe na uhusiano na uzao. Kuna tofauti kati ya unasaba na uraia. Yawezekana watu wa nasaba moja wakawa raia wa nchi tofauti vivyohivyo  watu wa  nasaba tofauti wakawa raia wa nchi  au taifa moja.Ushahidi ni Marekani. Kwa hiyo watu waelewe hili kuwa  unapozungumziwa uraia hauzungumziwi udugu wa damu bali  utambulisho. Mtu aweza kutambulika kuwa yeye kwasababu za kisheria  anatokea katika eneo la mipaka fulani, mtu huyohuyo kesho akawa mtu wa mipaka  mingine na keshokutwa mingine.

Rasimu pendekezwa  imeugawa uraia au utambulisho katika  makundi mawili. Kwanza uraia au utanbulisho wa kuzaliwa pili  uraia au utambulisho wa kuandikishwa. Ibara ya 65(2)  inanukuliwa  hivi Uraia wa Jamhuri ya Muungano ni wa aina mbili na utapatikana kwa njia ya kuzaliwa au kuandikishwa”.
Kila moja katika haya lina mazingira yake, mwongozo wake na hadhi yake kama inavyoelezwa hapa chini :

URAIA  WA  KUZALIWA.

Uraia wa kuzaliwa umegawanyika katika makundi matatu, nayo ni :
( a ) Ni uraia unaotokana na kuzaliwa ndani ya Jamhuri ya muungano iwe Zanzibar au Tanganyika .Uraia huu unaainishwa katika Ibara ya 67 ( 1 ).  Ieleweke kuwa si yeyote atakayezaliwa katika Zanzibar au Tanganyika  ataitwa Mtanzania isipokuwa  ataitwa Mtanzania ikiwa Baba au Mama ni Mtanzania au wote kama ni Watanzania. Ni kusema kuwa kama baba si mtanzania wala mama lakini mtoto kazaliwa ndani ya mipaka ya Jamhuri ya Muungano basi mtoto huyo hawezi kuwa Mtanzania.  Utaona wazi kuwa ili mtu awe Mtanzania katika  hili yamezingatiwa  mambo makuu mawili. Kwanza azaliwe ndani ya jamhuri  na hapohapo mmoja kati ya wazazi wake awe mtanzania au wazazi wote  wawe watanzania. Hali hiyo ikitokea anazaliwa mtu kwa utambulisho wa Mtanzania.

( b ) Uraia mwingine katika uraia wa kuzaliwa ni pale ambapo  mtu atazaliwa nje ya Tanzania  na hapohapo mmoja kati ya wazazi wake awe baba au mama  au wote wawili akawa ni mtanzania. Mwingereza aishiye Uingereza amezaa na mama mtanzania na wanaishi Uingereza mtoto huyo ni Mtanzania.  Baba wa Kitanzania aishiye Marekani amezaa na mama wa kimarekani na wanaishi marekani  mtoto wao atakuwa mtanzania. Baba  mtanzania , mama mtanzania  wote wanaishi Zambia mtoto wao  atakuwa Mtanzania. Hii ndiyo maana yake na  ruhusa hii inatolewa na Ibara ya 67( 2 ).
Hizo ndizo aina tatu za uraia wa kuzaliwa.

URAIA  WA  KUANDIKISHWA.

Uraia wa kuandikishwa nao umegawanyika sehemu tatu  kama ifuatavyo :
( a ) Mtu ambaye si mtanzania lakini amekuwa mkaazi wa Tanzania  na kutimiza masharti ya kisheria  ikiwa ataomba kuandikishwa kama raia wa Tanzania basi  ataweza kupata haki ya kuwa mtanzania wa kuandikishwa. Ni kusema tu kuwa wageni  ambao wamekaa nchini na kupata hadhi ya ukaazi  wanayo nafasi ya kuomba Utanzania.

( b ) Mtu anaweza kuomba kuwa raia wa Tanzania wa kuandikishwa ikiwa atakuwa amefunga ndoa na raia wa Tanzania na kudumu naye katika ndoa kwa kipindi cha miaka saba mfululizo. Raia wa Amerika ambaye anaishi Amerika lakini kamuoa Mtanzania na ameishi naye kwa kipindi cha miaka  saba mfululizo  anayo haki ya kuomba kuwa raia wa Tanzania. Hii haijalishi  ni kwa kuoa au kuolewa Mtanzania aliyeolewa na mme mgeni anaweza kuomba na mtanzania aliyeoa mke mgeni anaweza kuomba.

( c ) Mtoto aliye na umri wa chini ya miaka kumi na nane ambaye
wazazi wake si raia wa Tanzania, akiasiliwa na raia wa Jamhuri ya
Muungano, kuasiliwa kwake, kutawezesha mtoto huyo kuwa raia wa Jamhuri
ya Muungano wa kuandikishwa
Huu ndio uraia wa kuandikishwa.

MWENYE  ASILI  YA  TANZANIA   NA   AKAACHA  KUWA  RAIA WA  TANZANIA.

Ibara 69 ya rasimu  imependekeza kitu kingine kinacholenga kutambua baadhi ya watu . Nje ya nchi wapo watu wengi ambao  ni wazawa wa Tanzania , damu yao ni ya Tanzania lakini kwasababu mbalimbali hasa za kisheria wamelazimika kuacha uraia wa Tanzania. Kwa  mfano kuna walioolewa na kuoa nje ya nchi na sheria za kule zikawalazimisha kukana utaifa wa nchi kabla ya kuruhusiwa kuishi huko. Kimsingi ni wa Tanzania  isipokuwa ni sheria tu imewafanya kuwa raia wa nchi nyingine. Unakuta wana baba zao Tanzania, mama zao, dada , halikadhalika watoto. Rasimu hii inasema kuwa hawa hawatakuwa raia wa Tanzania wala hawatakuwa wageni kama wageni wengine isipokuwa  watapewa hadhi maalum ambayo itawatofautisha wao na wageni wengine wasio na asili ya nchi hii. Bila shaka jambo hili limeigwa kutoka India ambako wahindi walio nje ya India  lakini wana asili ya Uhindi hupewa hadhi maalum. Hata wahindi tunaowaona hapa kwetu wengine wamezaliwa Ifakara,Igunga na wengine ni viongozi katika  serikali , bunge na mahakama wakienda  India hupewa hadhi maalum.

HADHI   MAALUM   NININI.

Kwanza ni kupata kitambulisho ambacho si uraia wa Tanzania wala si kibali cha kuishi kama anachopewa mgeni mwingine.

Pili, hadhi maalum inaambatana na baadhi ya haki mfano kuruhusiwa kupata elimu,kudahiliwa vyuo vya elimu ya juu, kutotakiwa kuwa na visa anapoingia na kutoka nchini, kupata huduma nyingine za kijamii kama raia  na pengine kuruhusiwa kumiliki mali isiyohamishika kama ardhi lakini kwa kiwango chenye ukomo fulani labda eneo kidogo kwa ajili ya makazi tu.

Aidha kuna vitu ambavyo hawezi kuwa na haki navyo kama kupiga kura, kugombea au kupigiwa kura, kupata ajira serikalini hususan kwenye vyombo vya ulinzi na usalama na uhuru wa kumiliki ardhi kwa kiwango kikubwa au kisicho mipaka.
Hii ndio maana ya hadhi maalum.

URAIA  NI   WA   NCHI  MOJA.

Ibara ya 69 inasema kuwa  uraia ni  wa nchi moja. Mwanzoni ilipendekezwa uraia wa nchi mbili kama katika baadhi ya nchi.Hili lilikataliwa  na kama lingekubaliwa ingewezekana kuwa na Mmalawi, Mtanzania, Mkenya Mtanzania, Msomali Mtanzania n.k. Kwasasa utaamua ima uwe Mtanzania au raia wa nchi nyingine.Hakuna nafasi ya kuwa raia wa nchi mbili.

FAIDA  ZA IBARA  HIZI..

Tumeona hali  ilivyo kuanzia ibara ya 65 mpaka 69, swali la ni kitu gani kimezingatiwa katika kupendekeza  Ibara hizo kusomeka hivyo linajibiwa hapa chini:
( a ) Ulinzi na usalama umezingatiwa kwa mfano pale ambapo uraia wa nchi mbili unazuiwa. Ingekuwa rahisi mtu kufanya uhalifu hapa na akaenda kuishi kwingine ambako ana uraia sababu yuko huru. Hata kiongozi angeweza kufanya ufisadi wa haki za binadamu au mabilioni ya hela  kwakuwa ana uraia wa nchi nyingine anahamia huko kwa amani kwakuwa huko hatafukuzwa au muda wa kibali chake hautaisha kwakuwa ni raia. Pia kwa kiasi inaondoa uwezekano wa kuingiliwa kisiasa kwa kupandikiza watu ambao  wanalenga kutekeleza mikakati haramu ya kijasusi inayoweza kuratibiwa na nchi nyingine.

( b )Kuondoa matabaka kwakuwa baadhi ya watu  hasa wenye uraia wa nchi mbili wangeonekana  ni watu wa hadhi fulani kuliko wengine.Ni kuzalisha tabaka jipya la Watanzania asili na Watanzania mseto. Na ni ukweli usiopingika kuwa ni wenye uwezo wa kifedha tu ambao wangeliweza hili. Sitaki kuamini kuwa Mtanzania anayeishi chini ya dola moja angeweza kuwa na wazo la kupata uraia wa nchi nyingine. Kula kwenyewe shida halafu afikirie kupata uraia wa nchi nyingine, haiwezekani. Pengo la matabaka lingekua.

( c ) Sababu za kiuchumi. Matajiri wa nchi nyingine ndio wangechangamkia fursa hii ili wapate  kutanua  na kuogelea kwenye rasimali za nchi. Hakuna ambaye angeweza kushindana nao.Wangenunua maelfu na maelfu ya ekari za ardhi na wazawa haswa wangebaki kuwa manamba na walinzi wa maeneo hayo.Ananunua ekari alfu moja anaweka kijumba cha chumba kimoja kwa ajili ya Mtanzania kumlindia, isingekuwa sawa.

(  d ) Nasaba ya mtu mwenye asili ya Tanzania imelindwa pale ambapo  hata kama yuko nje ya nchi na ameolewa au kuoa  raia wa nchi nyingine mtoto yule aweza kuwa raia wa Tanzania pia pale inapotolewa heshima ya HADHI MAALUM. Damu ya kizalendo ya nchi  imelindwa.

IMEANDALIWA   NA  MAWAKILI  WA BLOG HII.
0784482959
0714047241





Share this article :

0 comments:

Post a Comment