Saturday, 7 February 2015

KATIBA MPYA YAWEKA BAYANA HAKI ZA MTUHUMIWA NA MFUNGWA .


NA  BASHIR   YAKUB   (MWANASHERIA  MWANDAMIZI).

Rasimu inayopendekezwa ili iwe katiba imebeba mambo mengi  mazuri. Yumkini yanayojulikana ni machache. Kwanini, sababu  I wazi, ni ajenda za kisiasa. Mambo mengi yamepigwa kumbo  na kumezwa na mambo machache sana. Mambo yahusuyo madarak na  ni mifumo ya nchi  yamekuwa ndio rasimu.

Rasimu ina ibara 189, ni Ibara zisizofika hata kumi zinazopigiwa kelele. Ni masikitiko makubwa kwakuwa zaidi ya ibara 170 zimetelekezwa, ni ibara yatima.Katika kupingana na hilo  blogi  hii inaeleza na kuchambua  Ibara mbalimbali za msingi sana ambazo  kwa namna moja au nyingine hazitamkwi katika ufalme wa wanasiasa. Ni leo tena ambapo tutagusa Ibara za 46, 47 na 33.Kwa pamoja Ibara hizi zinazungumzia haki ya mtuhumiwa anapokamatwa au kuwa kizuizini, na haki za wafungwa. Ni ibara muhimu sana.

MTUHUMIWA   NI  NANI.

Mtuhumiwa ni mtu anayehisiwa kuhusika katika uhalifu wa kijinai na akawa chini ya ulinzi katika mamlaka za kiusalama, mahakamani ikiwa kesi yake inaendelea  au nje kwa dhamana huku kesi ikiendelea.Hakuna mtuhumiwa isipokuwa lazima kuna jinai. Madai hayana mtuhumiwa yana Mdaiwa au Mlalamikiwa.Hivyo basi Ibara hizi zikizungumzia mtuhumiwa zinazungumzia jinai.

MFUNGWA NI NANI.

Aidha Mfungwa ni mtuhumiwa ambaye kesi yake imesikilizwa imeisha na amepatikana na hatia katika makosa yote au baadhi na sasa ameanza au tayari anatumikia adhabu.Hakuna mfungwa kabla ya hukumu na adhabu. Wanaozuiliwa katika magereza na hali hawajahukumiwa na kutangaziwa adhabu hao ni watuhumiwa au rumande(remandee).

HAKI   ZIPI   ZIMETOLEWA   KWA MTUHUMIWA   NA   MFUNGWA.

( a )Imeelezwa kuwa mtu aliyekamatwa na kuwekwa kizuizini anayo haki ya kuelezwa katika lugha anayofahamu sababu za kukamatwa,haki ya kukaa kimya na madhara au matokeo ya kuzumgumza lolote . Kimsingi hii si haki  ya kuwa umepewa isipokuwa ni haki iliyo moja kwa moja (automatic right). Inawezekanaje umweke chini ya ulinzi mtu halafu  umzungumzishe lugha asiyoifahamu. Ni kwanini sasa umemweka chini ya ulinzi na unategemea lipi kutoka kwake hali hamfahamiani kwa lugha.

Ukiangalia unaona kuwa ni haki  ambayo hata isingesemwa ilikuwa ni lazima iwe hivyo. Na kimsingi ndivyo ilivyo hata kabla ya hii rasimu. Ni kwanini sasa hili jambo liko hivi hata kabla ya rasimu  na linaigizwa tena katika  rasimu katiba.

 Ni kuwa jambo hata kama ni dogo au  lipo na huwa linafanyika kwa mazoea au kwa sheria nyinginezo likiingizwa kwenye katiba hupata  umuhimu maalum wa pekee na huleteleza wajibu wa kisheria kwa maana kuwa wapo watakaoanza kuwajibika kwalo. Msingi  wa kuelezwa katika lugha anayoifahamu mtuhumiwa katika rasimu umeshikamanishwa katika  vipengela  vitatu.

Kwanza  kumueleza mtu kwa lugha anayoifahamu Sababu za kukamatwa kwake, Pili haki ya kutotoa maelezo yoyote  na Tatu  athari,madhara au matokeo ya kutoa maelezo au kusema lolote.
Hii ni kuwa mtu aambiwe  kwanini amewekwa chini ya ulinzi . Habari za twende utajua kituoni hakuna.Sema mimi ni fulani ninakuweka chini ya ulinzi wewe fulani kwasababu unatuhumiwa kwa wizi wa silaha, kubaka , kufanya fujo n.k. Pili una haki ya kukaa kimya kama utaamua kufanya hivyo kwakuwa hatukulazimishi kuongea lolote, na tatu  aambiwe mtu kuwa lolote utalolisema kuanzia sasa litakuwa ushahidi na litatumika katika mahakama  kama ushahidi  wakosa unalotuhumiwa nalo.

Hii ndio madhara,athari au matokeo ya kusema lolote. Athari, madhara au matokeo ya kusema lolote ni kile ulichokisemsa kutumika mahakamani kama ushahidi, basi. Hivyo ni kusema kuwa utatakiwa uelezwe hayo matatu katika lugha unayoifahamu kama u mtuhumiwa. 

Askari akimweka chini ya ulinzi mzungu asiyejua Kiswahili  na mzungu akakubali lakini akazungumza maneno fulani ambayo ni ushahidi mzuri kwa alichowekewa chini ya ulinzi, maneno hayo pamoja na uzuri wake katika ushahidi hayataweza kutumika dhidi yake kwakuwa hakuwa ameelezwa haki hizi kwa lugha anayoijua wakati wa kukamatwa kwake.Vivyo hivyo kwa masai asiyejua Kiswahili na wengineo.

( b )Haki nyingine ni kuwa `mtuhumiwa au mfungwa anapokamatwa na kuwa kizuizini anayo haki ya msingi ya kuwasiliana na wakili wake au mtu mwingine yeyote ambaye kwake  anaweza kutoa msaada. Kama ni  kituo cha polisi au pengine popote ni lazima basi wahusika wamwezeshe waliyemkamata kuwasiliana na watu  wake.

Hii ni pamoja na kumpatia mawasiliano kama hana namna ya mawasiliano  au kama hakuna kabisa uwezekano wa mawasiliano eneo hilo basi waliomkamata wanawajibika  kufika  kimwili au kutuma ujumbe panapohusika ili  mtuhumiwa au mfungwa aweze kuwasiliana na mtu aliyemtaka. Ile habari ya huruhusiwa kuongea na mtu yeyote kwakuwa uko chini ya ulinzi mara eti unaweza kuharibu upelelezi hakuna.

( c ) Kutolazimishwa  kutoa maelezo ya kukiri kosa. Mchezo huu mahala pake haswa ni vituo vya polisi. Hutumika nguvu nyingi kumlazimisha mtuhumiwa akiri kosa ikiwa ni pamoja na kumtesa.Upo ushahidi mwingi watu wamerushwa kwa umeme, wameingizwa chupa sehemu za siri, kutandikwa mijeredi hiyo wala siyo adhabu tena  siku hizi, kuninginizwa kichwa chini miguu juu  na mateso mengineyo ya kuudhi na kudhalilisha kabisa.

Pia kumwambia mtu kwa kumshawishi kuwa sema ukisema ukweli nitakusaidia utoke au nitakufutia kosa na mtu akalazimika kusema kama mwanausalama anavyotaka ili ajinasue nako ni kumlazimisha kukiri kosa kwa mujibu wa ibara hii. Ili isiwe kulazimishwa huna haja ya kumshawishi mtu, yatosha kumweleza kosa na kumuuliza kama analikubali au kulikataa.

( d ) Haki ya kufikishwa mahakamani haraka na mapema iwezekanavyo. Mahakama ndio hutoa  haki kwa kusema huyu anakosa au hana. Polisi,polisi jamii, mgambo , raia wema kazi yao ni moja tu kukamata na kumfikisha mahakamani. Hawaruhusiwi kukaa na mtuhumiwa kwakuwa kisheria wakishamkamata hawana kazi naye.

Kazi gani watafanya naye baada ya kumkamata, haipo. Hali hii ndo inalazimisha  mtuhumiwa kufikishwa haraka mahakamani . Kama ni maeneo ya mijini au sehemu ambapo mahakama ipo karibu ndani ya masaaa 24 yatosha mtuhumiwa kufikishwa mahakamani, na kama ni vijijini , kama mtu anakamatwa leo,  siku hiyohiyo au kesho kutokana na hali usafiri mtuhumiwa asafirishwe mpaka ilipo mahakama.

( c ) Haki ya kuwekwa katika mazingira yanayozingatia haki za binadamu. Sero zenye mikojo na vinyesi,wadudu wachafu wa kila aina, sasa zitakuwa haramu. Imezoeleka hivyo mpaka sasa watu wanajua kuwa maana ya kuwekwa ndani ni ukutane na mazingira magumu ili ujutie kosa.Eti hiyo ndio ndani(sero). Sivyo hata kidogo, kuwekwa ndani ni kusubiria tu taratibu za kisheria ambako hakuna uhusiano na kuwekwa sehemu chafu. Inawezekana mtuhumiwa kukalishwa hata  kwenye sofa na vigae kwani haiharibu chochote, haiingilii upelelezi, wala haitamfanya ashinde au ashindwe mahakamani. Sehemu chafu ni tabia mbaya za kinazi (Nazism),mateso na kutojali haki za watu.

( e ) Mtu anayetumikia kifungo anayo haki pia ya kupatiwa nakala ya hukumu na mwenendo wa kesi yake ili basi imwezeshe kukata  rufaa kama yu tayari kufanya hivyo au kuchukua hatua nyingine atakazoona ni stahiki na zenye kufaa.Gharama za upatikanaji wa nakala ya hukumu na mwenendo wa kesi haziko juu ya mfungwa isipokuwa mamlaka zinazomshilikia ndizo zitahusika na hili. Hii ni kwasababu hukumu na mwenendo wake hupatikana kwa gharama  mahakamani.Haki nyingine za mfungwa ni kama nilivyozieleza hapo juu.

FAIDA  KATIKA  IBARA  HIZI.

(  a ) Awali ya yote ni kuwa baadhi ya mambo hayakuwa katika katiba lakini  yalikuwa yakifanyika sawasawa kabisa na rasimu inavyoeleza. Umuhimu ni kuwa mambo hayo sasa yatakuwa rasmi na tutayapata katika katiba kama itapita. Umuhimu wake nini. Jambo linapoingia katika katiba linapata hadhi ya pekee na linaibua ulazima katika wajibu wa kulitekeleza.

 Mathalan tumeona hizo haki juu , hii ina maana kuwa  mtuhumiwa au mfungwa ambaye atatendewa kinyume anayo haki sasa ya kufungua shauri la madai na kudai fidia jambo ambalo lisingewezekana kama mambo haya hayapo ndani ya katiba. Kama ni magereza anamfungulia shauri mtu hasa aliyemtendea kinyume, anaiunganisha magereza na mwanasheria mkuu wa serikali  na kama ni polisi anamweka askari hasa aliyemtesa, analiunganisha jeshi la polisi na mwanasheria mkuu wa serikali.

Kwa kuwashitaki wahusika mateso yanaweza kupungua kwakuwa serikali itajikuta ikilipa mamilioni ya fedha kama fidia mara kwa mara. Kwahiyo wakuu wa usalama watawatahadharisha watendaji wao ili kuepuka migogoro  na kunusuru mamilioni  ya shilingi.Hii ni kusema kuwa kuteswa sasa yaweza kuwa kazi nzuri  yakupatia mtaji au kutoka kimaisha.

( b ) Pia inaposemwa kuwa mtuhumiwa au mfungwa aelezwe shitaka au mwenedo wa kushauri kwa lugha anayoifahamu hili linakwenda  mpaka katika nakala ya hukumu. Sheria ya sasa lugha ya mahakama hasa kuanzia mahakama ya wilaya ni kiingereza. Hii ni katika kuweka kumbukumbu lakini mambo mengine inatumika lugha wanazofahamu wahusika. Inaposemwa lugha ya kumbukumbu ni kiingereza ina maanisha kuwa hukumu zote na mienendo lazima iwe kwa kiingereza.

Kwa ibara hii utawekwa utaratibu sasa au yatafanyika mabadiliko ili kuwawezesha wafungwa na  wengine kupata nakala za hukumu kwa lugha wanazofahamu hususan Kiswahili. Ni jambo jema kwakuwa ilikuwa mtu akipata nakala ya hukumu lazima amtafute mkalimani.

( c ) Haki nyingine ni mfungwa na mtuhumiwa kukaa mazingira safi na salama  ambalo limekuwa jambo la msingi kwakuwa limezingatia ubinadamu. Niseme jambo moja tu kuwa haki ya ubinadamu yaani kwamba  fulani ni binadamu hakuna wa kuiondoa. Ni haki anayoitoa mungu tu.

Ni haki ya kuzaliwa ambayo mtu hawezi kupewa na mtu mwingine. Ni haki ambayo huwezi kuifananisha na haki nyingine yoyote. Ina thamani kubwa na kuiondoa au kujaribu kuifubaza au kuiua kwa kumweka mtu sehemu zenye mikojo na wadudu ni kinyume kabisa cha uungwana.Si kumdhalilisha yule pekee isipokuwa ni kuudhalilisha ubinadamu kwa ujumla wake  akiwemo yeye anayetekeleza ubaya huo.

0784482959
0714047241




Share this article :

0 comments:

Post a Comment